16 September 2016

ONDOA WASIWASI, PALE ULIPOSHINDWA ANZA UPYA, PALE ULIPOLIZWA FUTA MACHOZI, PALE ULIPOCHAFUKA SAFISHA UPYA, MAISHA YANAENDELEA



Nimeweka picha hii ya rafiki yangu na dada yangu katika Bwana maana ni mtu mwenye ushuhuda mkubwa lakini hakati tamaa. Nimejifunza mengi kutoka kwa dada huyu.

Nianze kwa kusema kwa mfano huu;
Mwanamke mmoja ambaye baada ya kufiwa na mume wake, alianza kujiona mpweke na kuvunjika moyo. Siku moja alipokuwa akitoka shuleni alikokuwa akifundisha, alianza kufikiri na kujisemea moyoni mwake kuwa shule aliyopo ni ya kimaskini, pia barabara anayopita wakati wa kwenda na kurudi nyumbani kwake ni mbaya, hivyo aliamua kuchukua uamuzi wa kujinyonga.
Alifikia hatua hiyo baada ya kuona kila kitu kwake hakiwezekani. “Sioni faida ya kuishi. Ninaamka kila asubuhi, kukabiliana na maisha. Nina hofu ya kila kitu, hofu ya kutokumpata tena mtu sahihi wakunioa, hofu ya kutoweza kumudu kuliendesha gari langu, hofu ya kushindwa kulipa kodi ya nyumba, hofu ya kutokuwa na chakula cha kutosha. Nina hofu ya afya yangu nami sina fedha ya kumwona daktari.
"Yote hayo yalimfanya kufikiria kujinyonga. Siku moja alisoma kifungu kimoja kilichomuinua kutoka katika ile hali iliyokuwa inamkabili na kumpa moyo wa kuendelea kuishi. Kifungu alichosoma kilisema: "Kila siku ni maisha mapya kwa mtu mwenye busara."
Alikiandika kifungu kile na kukibandika kwenye kioo cha gari yake alipoweza kukiona kila mara alipokuwa akiendesha.
Aligundua kuwa kuishi si jambo gumu kama alivyofikiria awali, alijifunza kusahau yaliyopita na kutokufikiria mambo ya kesho. Kila siku alijisemea moyoni mwake kuwa, ‘leo ni siku mpya’.
Alifanikiwa kuishinda hofu iliyokuwa ikimkabili ya upweke aliyojitakia. Tangu hapo akawa mtu wa furaha, mwenye mafanikio na anayependa kuishi.
Kuanzia hapo alisema kuwa hataogopa tena, bila kujali maisha yatakuwa ya aina gani kwake. Aligundua kuwa hataogopa maisha yajayo na ndiyo maana kila siku ni mpya kwa mtu mwenye busara.

JINSI YA KUONDOA WASIWASI
Kumbuka kuwa hali ya wasiwasi inakuondolea uwezo wa kufikiri. Kwani unapokuwa na hofu akili yako 'inaruka' na kufikiri hapa na kule na kila mahali, na unapoteza nguvu yote ya maamuzi. Hata hivyo, wakati unapojilazimisha kufikiria jambo linalokufanya upatwe na hali hiyo na kuikubali katika akili yako, unaiweka katika kupata muafaka wa jambo linalokukwaza.
Unapokuwa na wasiwasi unaweza kupata vidonda vya tumbo, pia uzito wako unaweza kupungua ghafla pamoja na kupata maradhi mbalimbali. Ili kuondokana na hali hiyo, inakupasa kuacha kufikiria na kujipa ujasiri katika kila jambo unalolifanya, pamoja na kuamua kufanikisha mipango yako ya baadaye. Pia unaposafiri maeneo mbalimbali inakusaidia kukutana na watu tofauti na kupata mawazo mapya ya maisha hivyo kujikuta unaondokana na hali uliyokuwa nayo.
“Hofu inasababisha wasiwasi. Pia wasiwasi huo, unakufanya uwe katika hali ya kutotulia na ya fadhaa, huathiri misuli ya tumbo lako, hubadili tumbo lako kutoka katika hali ya kawaida, ambayo mara nyingi huchangia kupata vidonda vya tumbo,”.
Naye Dk. Joseph Montague anasema huwezi kupata vidonda vya tumbo kutoka kwenye kile ulacho, bali unapata vidonda hivyo kutoka kwa kile kinachokutafuna.
Hofu, wasiwasi, chuki, ubinafsi na kutokuwa na uwezo wa kukabiliana na ukweli wa mambo katika ulimwengu huu, ni sababu kubwa za maumivu ya tumbo, pamoja na vidonda…vidonda vya tumbo vinaweza kukuua. Pia utafiti uliofanywa umebaini kuwa wafanyabiashara wengi ambao hawajafikisha miaka 45 hupatwa na magonjwa ya moyo, vidonda vya tumbo na shinikizo la damu, kutokana na kuishi maisha ya wasiwasi. Mtu anaweza kupata mafanikio katika biashara yake na kujisababishia matatizo makubwa ya afya yake. Itamsaidia nini kupata ulimwengu wote kwa utajiri na kupoteza afya yake? Hata kama amekuwa tajiri wa dunia inambidi alale katika kitanda kimoja kwa wakati na kula mlo mara tatu kwa siku, siyo kujishughulisha kupita kiasi na kusahau muda wake wa kula, pamoja na kulala.
Zaidi ya nusu ya wagonjwa wanaolazwa hospitalini huwa na matatizo yaliyosababishwa na hofu, wasiwasi, mshtuko, dukuduku na hali ya kutofanya lolote la maana. Mtu mmoja alisema kuwa kosa linalofanywa na wataalamu wanakuwa wanajitahidi kuponya mwili, badala ya kuangalia chanzo cha tatizo na kukishughulikia. Ingawa mwili na ufahamu ni mmoja na hautakiwi kutenganishwa.
Wasiwasi unaweza kukuweka kwenye kiti cha walemavu kutokana na ugonjwa wa viungo na ugonjwa wa baridi yabisi. Dk. Russell Cecil ameorodhesha vitu vinne vinavyochangia ugonjwa wa baridi yabisi kuwa ni: kuvunjika kwa ndoa, majanga ya kutokuwa na fedha pamoja na huzuni, upweke na wasiwasi pamoja na hali ya kutaka kupata faraja kuchukua muda mrefu tofauti na matarajio.

Asante kwa kusoma ujumbe huu. Kwa ushauri zaidi tembelea kituo chetu cha ushauri kilichopo Ukonga. Lakini pia utakua ukinisikia hivi karibuni kupitia Sibuka Fm.
Pia unaweza ukarekodi tatizo lako kwa ufupi ukanitumia kwenye namba yangu ya whatsap 0716560094, nitakusaidia.

0 comments:

HEART OF WORSHIP

HEART OF WORSHIP