26 December 2012

PADRI wa Kanisa Katoliki Mjini Zanzibar amepigwa risasi




PADRI Ambrose Mkenda wa Kanisa Katoliki, Mjini Zanzibar amepigwa risasi na watu wasiojulikana nje ya nyumba yake juzi saa 1:45 jioni wakati akitokea kanisani.
Hili ni tukio la kwanza katika historia ya Zanzibar kwa kiongozi wa kanisa kushambuliwa wakati wa Krismasi, lakini ni tukio la pili kwa kiongozi wa dini kushambuliwa mwaka huu.
Hivi karibuni, Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Soraga alimwagiwa tindikali iliyomjeruhi vibaya usoni na kifuani na watu wasiojulikana. Shambulio hilo lilimlazimu kiongozi huyo kwenda kutibiwa India ambako ameambiwa anapaswa kuripoti hospitalini kila baada ya miezi sita.
Habari zilizopatikana jana zimeeleza kuwa Mkenda ambaye ni Paroko wa Parokia ya Mpendae, alipigwa risasi begani na shingoni na afya yake si nzuri.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Aziz Juma Mohammed alisema jana kuwa majeraha hayo yamemsababishia kutokwa na damu nyingi.
Alisema baada ya shambulio hilo, Padri Mkenda alipelekwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, Zanzibar. Hata hivyo, padri huyo alisafirishwa kwa ndege jana hadi Dar es Salaam ambako amelazwa katika chumba cha Wagonjwa Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU), katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.


Kamanda Aziz alisema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo, lakini akabainisha kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa alipigwa risasi baada ya watu hao kumshuku kuwa alikuwa na fedha za sadaka.
“Father Mkenda kitaaluma ni mhasibu na amekuwa akishika makusanyo ya fedha pale kanisani. Sasa huenda wahalifu hao waliona amechukua fedha na ndipo walipomfuata na kumpiga. Lakini hata hivyo, huo bado ni uchunguzi wa awali tu,” alisema Kamanda Aziz na kuongeza:


“Waliofanya tukio hili wamelifanya kwa madhumuni gani, ni swali gumu kujua sasa. Inawezekana kuna mambo mengine zaidi ya watu hao kutafuta fedha. Uchunguzi ukimalizika tutajua cha kufanya.”


Kamanda Aziz alisema walipata taarifa za tukio hilo saa 2:00 usiku na polisi walikwenda katika eneo hilo la Francis Maria anakoishi Padri Mkenda.


“Tulipofika tukakuta maganda mawili ya risasi za bastola na upande wa kulia wa kioo cha gari yake (padri) kuna damu katika viti vyake,” alisema Kamanda Aziz.
Alisema baadaye padri huyo alipelekwa hospitalini kwa ajili matibabu ambako madaktari walifanikiwa kumtoa mabaki ya risasi mwilini kabla ya jana kupelekwa Muhimbili.
“Tumempokea padri huyo saa 4:20 asubuhi leo (jana). Tulianza kumchunguza afya yake, baadaye kumfanyia uchunguzi kisha kumchukua kipimo cha CT Scan ili kubaini ilipo risasi hiyo,” alisema, mkurugenzi wa zamu katika hospitali hiyo, Agnes Mtawa.


Source: Mwananchi

0 comments:

HEART OF WORSHIP

HEART OF WORSHIP